BAADA ya ratiba ya ligi kuu kuwekwa wazi kuwa itaanza kuunguruma Agosti 22, mwaka huu, mshambuliaji wa Simba, Meddie Kagere raia wa Rwanda ameweka bayana kuwa atapambana vilivyo kwa ajili ya kuifanya timu hiyo iweze kutetea ubingwa wa ligi hiyo ikiwa ni baada ya kulikosa taji la Kagame Cup.
Kagere aliyetua Simba akitokea Gor Mahia ya Kenya, atakuwa sehemu ya kikosi cha Simba ambacho kitaanza kampeni ya kutetea ubingwa huo walioutwaa msimu uliopita kwa kucheza na Prisons, mchezo utakaopigwa Agosti 22 kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar.
Straika huyo ambaye anatarajiwa kuunda utatu na wachezaji Johh Bocco na Emmanuel Okwi, atakuwa mmoja wa watakaoenda nchini Uturuki kwa ajili ya kambi ya kujiandaa na msimu ujao.
Kagere ameliambia Championi Ijumaa, kuwa anajipanga vilivyo kuisaidia Simba kutetea ubingwa wake kwa msimu wa pili ambapo uhakika wa kufanya hivyo atakuwa nao baada ya kutoka katika kipindi cha pre season ambacho wao watakuwa Uturuki.
“Kwangu kwanza nasikitika kulikosa taji la Kagame Cup hivi karibuni lakini niseme kwamba tutarekebisha kila kitu hivi karibuni. Hatutaki kuona tunapoteza tena taji lingine kama timu na kwangu naamini tutajipanga kutetea mataji yote ambayo yatakuwa mbele yetu.
“Kwangu ninaamini wakati wa kujiandaa na ligi ‘pre season’ kitakuwa kipindi cha kurekebisha makosa yetu pamoja na kujuana na wachezaji wengine ambao walikuwa mapumziko. Kwa kikosi hiki mimi naona kabisa wapinzani wetu hawataweza kutuzuia kwa namna yoyote ile,” alisema Kagere.
0 Comments:
Post a Comment