Sunday 22 July 2018

Wagombea 30 CCM wapita bila kupingwa


Tume ya  Taifa ya Uchaguzi, imetangaza kuwa jumla ya wagombea 30 wa Udiwani katika uchaguzi mdogo wa kata 77 utakaofanyika Agosti 12, mwaka huu, wamepita bila kupingwa.  

Akizungumza Jijini Dar es Salaam Mkurugenzi wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC), Dkt. Athumani Kihamia amesema kuwa wagombea hao wamepita bila kupingwa baada ya Tume kukutana, kujadili na kuyatolea uamuzi mapingamizi mbalimbali yaliyoweka na wagombea wa udiwani. 

Amesema madiwani wote waliopita bila kupingwa wanatoka Chama cha Mapindizi (CCM) na kuongeza kuwa rufaa zilipokelewa na kujadiliwa kwa kuzingatia matakwa ya kifungu cha 44(5) cha Sheria ya Uchaguzi ya Serikali za Mitaa, Sura ya 292, kikisomwa pamoja na Kanuni ya 28(1)(2) ya Kanuni za Uchaguzi wa Serikali za Mitaa (Uchaguzi wa Madiwani) za mwaka 2015. 

“Tume, ilipokea, ilijadili na kufanya maamuzi ya Rufaa 25 ambapo jumla ya wagombea kumi (10) walifanikiwa na hivyo kuendelea na uchaguzi na wagombea 15 rufaa zao hazikufanikiwa na hivyo kutoendelea kuwa wagombea,” alisema Dkt. Kihamia.

0 Comments:

Post a Comment