Thursday, 22 April 2021

Kocha Mkuu wa Simba atamani kubaki na Kikosi hiki Msimu hujao

Kocha Mkuu wa Simba Didier Gomes amesema anatamani kuwa na wachezaji wake wote alionao sasa katika msimu ujao wa 2021/22

Gomes aliyetua Simba mwezi Januari 2021, ametengeneza kikosi imara ndani ya muda mfupi

Amefanikiwa kutinga robo fainali ya michuano ya ligi ya mabingwa barani Afrika tena akiwa kinara wa kundi A

Aidha uimara wa kikosi chake unampa uhakika wa kutetea ubingwa wa ligi kuu kwa msimu wa nne mfululizo pamoja na michuano ya kombe la FA

Hata hivyo mafanikio haya ya Simba yameongeza soko kwa wachezaji wake muhimu ambao tetesi zinashika kasi kuwa ziko timu zinataka kuwasajili

Gomes amesema angependa kuingia msimu ujao akiwa na timu hii aliyonayo sasa kwani ana uhakika watafanya vizuri

"Sijafahamu ni wachezaji gani wanaweza kuondoka lakini nikuhakikishie nawapenda wachezaji wangu, nahitaji kubaki nao kwa misimu mingi ijayo"

"Ni jambo zuri kutengeneza timu nzuri kwa misimu mingi ijayo. Nataka niwe nao wote kwa misimu miwili, mitatu au minne ijayo kwa ajili ya kujenga timu bora zaidi.

"Nina wachezaji wazuri ambao najivunia kufanya kazi nao," alisema Gomes

Miongoni mwa wachezaji ambao wanawindwa sana na vigogo barani Afrika ni mlinda lango Aishi Manula ambaye mkataba wake na Simba unamalizika mwishoni mwa msimu

Jana baada ya mchezo dhidi ya Kagera Sugar, Manula alisema kuwa mafanikio aliyopata yanampa sababu ya kutaka kusaka changamoto nje ya nchi

Hata hivyo amesisitiza klabu ya Simba ndio itaamua hatma yake

0 Comments:

Post a Comment